WAOMBOLEZAJI WAFUKUZWA MOCHWARI

 

KUTOKANA  na janga  la  Corona    kuendelea  kutikisa   maeneo mbali mbali ya  nchi na dunia ,mkuu wa  mkoa wa Iringa  Queen  Sendiga amelazimika  kuwatimua  waombolezaji  ambao walikuwa  wamefurika katika  chumba  cha  kuhifadhia maiti  Hospitali ya  Rufaa ya  mkoa wa Iringa  kwa  ajili ya  kufuata miili ya  ndugu  zao .

Mkuu  huyo  wa  mkoa   alifika  eneo  hilo la chumba  cha kuhifadhia maiti  baada ya  uongozi wa Hospitali  hiyo  kueleza  kero ya  wananchi  kusongamana katika  eneo hilo  kinyume na maelekezo ya  wizara ya  afya .

Akielezea  sababu ya  kuwafukuza  waombolezaji hao  amesema    hali ya janga la UVIKO-19  ndani ya  mkoa wa Iringa ni  kubwa na  hivyo  lazima  kila mwananchi kuchukua tahadhari  kwa  kuzingatia maagizo ya  wizara ya  afya na moja ya maagizo hayo ni misongamano isiyo ya  lazima .



" Naomba  kuagiza  kuanzia leo hii  watakaoruhusiwa  kufika chumba cha  kuhifadhia maiti  kuchukua mwili ni  watu wanne pekee na sio zaidi ya hapo  walinzi  hakikisheni hapa nje  hakuna  msongamano wowote wakati  wote  hebu tazama  hapa  leo zaidi ya  watu 100  wamekaa nje ya chumba  cha  kuhifadhia maiti na hao  wamefuata  mwili  mmoja tu na jiulize  hawa  wote wamekuja  kubeba mwili  huu mmoja hapana  haiwezekani kuacha misongamano kama  hii"  alisema huku akiwataka  wafiwa  hao kuanza kutawanyika eneo hilo.

Pia ameagiza ofisi ya  mkurugenzi wa Halmashauri ya manispaa ya  Iringa  kutumia vyombo vya habari  kutangazia  wananchi juu ya  kuepuka mikusanyiko  katika eneo  hilo na maeneo mengine  na akaagiza  wale wanaokwenda  kuona  wagonjwa   wasizidi  zaidi ya  wawili  kwa  mgonjwa mmoja .

Mganga mfawidhi wa hospitali ya rufaa ya mkoani Iringa Dkt  Alfredy Mwakalebela  amesema kumekuwepo na changamoto kubwa  sana katika  eneo hilo la chumba  cha kuhifadhia maiti  kwa  wananchi  kulazimisha kuingia getini  kusubiri  miili ya  jamaa  zao .

Kwa  upande  wake kamanda wa  Polisi wa mkoa wa Iringa  Juma Bwire  ameagiza  mmiliki wa kampuni   inayohusika na ulinzi katika Hospitali ya  Rufaa ya mkoa wa Iringa  kufika ofisini kwake  ili  kupewa maelekezo  ya nini cha  kufanya kwa  ajili ya kuthibiti  misongamano katika eneo hilo la Hospitali ya  rufaa ya mkoa wa Iringa .


Post a Comment

0 Comments