Na Adrian Audax - Mwanza

Mkuu wa kituo cha Nyakato Dastun Kombe ametoa taarifa ya uwepo wa vitendo vya ukatili katika maeneo mbalimbali ya jiji la Mwanza,

Taarifa hiyo imewasilishwa katika kikao maalum cha halmashauri ya Chama Cha Mapinduzi ambacho kimehudhuriwa na wajumbe wa kamati ya siasa, wajumbe halmashauri kuu, wenyeviti wa mtaa, watendaji wa vijiji, wakuu wa shule za misingi na sekondari, Jopo la wataalamu, Madawati ya kijinsia pamoja na Jeshi la polisi


Kombe amesema kuwa ndani ya siku Tatu watoto watatu wenye umri chini ya miaka minne wamefanyiwa matukio ya kikatili katika kata ya Mahina na Mhandu, huku akieleza kuwa watoto hao walichukuliwa kwa madai ya kwamba wanaenda kununuliwa pipi lakini kwa hali isiyo ya kawaida hufanyiwa vitendo vya ubakaji na watu hao,

Pia ameongeza kuwa kuna tukio lilifanyika Maeneo ya Shibula ambapo mtoto wenye umri wa miaka 2 na mwezi 1 alibakwa, Pia katika eneo la  Iyabo mtoto wenye umri wa miaka 3 na mwingne mwenye umri wa miaka 4 walifanyia ukatili huo ambapo Watoto wote wamefikishwa katika vituo vya afya na matibabu yanaendelea.


Mkuu wa upelelezi wilaya ya Nyamagana Inspekta R. Mapungu  amesema kuwa Jeshi la polisi tayari limeanza msako wa kuwabaini waharifu katika mitaa yote na zoezi hilo linafanyika pia kupitia mikutano ya hadhara inayoandaliwa na serikali ya kata,

Naye Mbunge wa Jimbo la Nyamagana Mhe. Stansilaus Mabula ameonesha kusikitishwa na taarifa hizo za kikatili na kuwataka wazazi pamoja na walezi wa watoto kutoa ushirikiano kwa Jeshi la polisi ili kubaini waharifu hao na kuwachukulia hatua za kisheria.

Akitoa Ushauri kwa wazazi ili kuepusha mazingira ya vitendo hivyo  Mstahiki Meya wa halmashauri ya Jiji la Mwanza Mhe, Sima Costantine amewataka wazazi kuwajengea watoto wao mazingira ya kutozurula  ovyo pia   amewataka wenyeviti wa vitongoji kuandaa mikutano kwa kushirikiana na Jeshi la polisi ili kutoa elimu juu ya ulinzi wa watoto,