WASHUKIWA 7 WASHIKILIWA NA POLISI KWA KUANDAA CHAKULA CHENYE SUMU

Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt.Binilith Mahenge 

Watu 50  wa Kata ya Unyambwa kijiji cha Kisasida katika Manispaa ya Singida mkoani Singida   wamenusurika kifo baada kula chakula kinachosadikika kuwa na sumu katika shughuli za ufunguzi wa Madrasa kijijini hapo ambapo katika tukio hilo mtoto mmoja mwenye umri wa miaka 7 amefariki dunia.

Kufuatia tukio hilo Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt.Binilith Mahenge amewatembelea wananchi hao waliolazwa katika hospitali ya mkoa huo na kuwapongeza madaktari wa Hospitali hiyo kwa jitihada za kuhakikisha wananusuru maisha ya wananchi hao ambapo kwa sasa hali zao zinaendelea vizuri na kuipongeza Serikali kwa kuweka miundombinu mizuri ya huduma katika sekta ya afya.

Kwa mujibu wa Mganga mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa Banuba Deogratius amesema walipokea jumla ya wagonjwa 50,kati yao Wanawake 34 na Wanaume 16 ambapo hali zao zinaendelea vizuri na wameanza kuwaruhusu baadhi yao kurudi nyumbani kuendelea na majukumu yao.

Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida Stella Mutabihirwa amesema wanawashikilia washukiwa 7 walioshiriki kuandaa chakula hicho kwa ajili ya uchunguzi na tayari wamechukua chakula hicho kwa uchunguzi zaidi.

Katika tukio hilo Kamanda amesema mtoto mmoja mwenye umri wa miaka (7) ambaye amefahamika kwa jina la Fahad Masudi amefariki dunia kabla ya kufikishwa hospitali kwa ajili ya kupatiwa matibabu.

Post a Comment

0 Comments